Quantcast
Channel: AMKA MTANZANIA
Viewing all articles
Browse latest Browse all 1010

Mambo Saba (07) Yatakayokuwezesha Kufikia Utajiri Kupitia Ujasiriamali.

$
0
0
Hivi majuzi, jarida maarufu kwa kuandika kuhusu fedha, mafanikio na biashara la nchini 

Marekani, Forbes, lilitoa orodha ya watu matajiri sana duniani. Kwa mwaka huu 2017, pamekuwepo na watu wapya 195 ambao wametangazwa kuwa mabilionea. Sasa hiyo siyo habari muhimu hasa kwa tunachokwenda kujadili leo, bali habari muhimu sana ni hii; robo tatu ya mabilionea hao wapya ni wajasiriamali ambao walianzia chini kabisa. Yaani walianza bila ya kitu kabisa, hawakurithi mali wala kushinda bahati nasibu, badala yake walipambana wakianzia chini kabisa na hatimaye kuweza kufanikiwa sana.
 

Inawezekana lengo lako siyo kuwa bilionea, lakini kitu kimoja ambacho nina uhakika nacho kuhusu wewe ni kwamba unahitaji utajiri. Unahitaji kuwa na uhuru wa kifedha ili uwe huru kwenye maamuzi yako ya kimaisha. Hivyo basi, kwenye makala ya leo nakwenda kukushirikisha mambo saba muhimu yatakayokuwezesha kufikia utajiri kupitia ujasiriamali. 

Naomba uelewe msisitizo hapa ni kupitia ujasiriamali, maana njia hii ndiyo inazalisha matajiri wengi zaidi kwenye zama hizi.

Mambo hayo saba ni kama yafuatayo;

1. Jifunze kuwaamini watu.

Hutaweza kufikia utajiri kupitia ujasiriamali iwapo kila kitu utafanya mwenyewe. Vitu vingi unavyofanya unahitaji kuwapa wengine wakusaidie na wewe uweke nguvu zako kwenye yale ambayo ni muhimu zaidi. Sasa kama huwezi kuwaamini watu na kuona wanaweza kufanya kazi nzuri, hutaweza kuwapa majukumu yako na badala yake utang’ang’ania kufanya kila kitu peke yako na kuishia kushindwa.

Jifunze kuwaamini watu na wape majukumu ambayo wanaweza kukusaidia. Kufikia utajiri unahitaji msaada wa wengi, jua namna ya kufanya kazi vizuri na watu wengi.

SOMA; Upotoshaji Mkubwa Unaofanywa Kwenye Elimu Ya Ujasiriamali.

2. Fanya vizuri sana kile ulichochagua kufanya.

Hakuna tajiri ambaye anafanya mambo kwa kubahatisha. Wote ambao wanafanikiwa sana kwenye ujasiriamali wanafanya vizuri sana kile ambacho wamechagua kufanya. Wanaweka juhudi kubwa kuongeza thamani na kutengeneza matokeo bora kabisa. Kwa njia hii watu wanawaamini na kuwategemea kupitia kile wanachofanya.

Jitengenezee jina kwa kufanya vizuri sana kile ambacho umechagua kufanya. Hakikisha kuna kitu kinakutofautisha wewe na wengine ambao wanafanya kama unachofanya wewe.

3. Toa zaidi ya unavyotegemea kupokea.

Badala ya kuuliza dunia inakupa nini, jiulize unaipa nini dunia. Haijalishi wateja wanakulipa kiasi gani, hakikisha unawapa vitu vyenye thamani kubwa, vitu ambavyo ni bora kabisa. 

Hakikisha mteja akiangalia anachokulipa na unachompa, anaona kama amekuibia. Na wala siyo lazima uingie hasara kwenye kufanya hivyo, inaweza kuwa ni ile huduma ya kipekee kabisa anayoipata, ambayo hajawahi kuipata kwingine popote.
Ipe dunia zaidi ya unavyotegemea kupata, na dunia italazimika kukulipa wewe kwa kadiri ya unavyotoa.

4. Sahau majuto.

Utafanya makosa mengi sana kwenye safari yako ya ujasiriamali, ambayo yatakukwamisha kufanikiwa. Lakini kupoteza muda kufikiria makosa hayo ya nyuma, hakutakuwa na msaada wowote kwako. Kujutia yale uliyofanya na yakakurudisha nyuma, ni kupoteza muda wako.

Kwa makosa yoyote ambayo ulishafanya, jifunze na songa mbele. Una mengi sana ya kufanya ambayo yapo mbele yako, usipoteze muda kuangalia nyuma, badala yake kazana kusonga mbele.

5. Jifunze kukubali kupoteza.

Hakuna mtu anayeshinda kila wakati. Hata wajasiriamali unaowaona wana mafanikio makubwa, kuna wakati walishindwa, kuna wakati walipoteza. Kabla hujafanikiwa, utapitia vikwazo na changamoto nyingi. Lazima ukubali kupoteza na kujifunza ili kuweza kusonga mbele.

Pale unapoanguka usikae chini na kusema kwa nini mimi, badala yake kubali kilichotokea na simama kusonga mbele. Wale wasiokubali kupoteza hutafuta mtu wa kumlaumu kwa kilichotokea, wale wanaofanikiwa wanakubali, wanajifunza na kisha wanasonga mbele, wakifanya kwa ubora zaidi.

SOMA; Njia TATU Za Kufanya Moto Wa Ujasiriamali Uendelee Kuwaka Kwenye Nafsi Yako…

6. Chukua jukumu la maisha yako na mafanikio yako.

Hakuna ambaye atakuja kukutoa hapo ulipo kama wewe mwenyewe hutaamua kutoka hapo. 

Na hata unaposhindwa, usikimbilie kutafuta nani kasababisha, hakuna mkono wa mtu yeyote ila wako, ambao unapelekea wewe kushindwa. Hivyo shika jukumu la maisha yako, pambana kufikia ndoto zako. Hakuna atakayekuletea utajiri mezani, na wala hakuna njia ya mkato ya kuufikia. Lazima ukubali kuweka kazi na muda wa kutosha ili kupata kile unachotaka.

7. Una vitu viwili tu, NENO lako na JINA lako.

Jifunze kuwa mwadilifu na mwaminifu, kila neno lako linabeba jina lako. Jifunze kutimiza kile ambacho unaahidi. Hakikisha matendo yako yanaendana na maneno yako. Unahitaji kujijengea uaminifu usiotiliwa shaka, ili watu waweze kukuamini na kufanya biashara na wewe na hata kukusaidia. Usijihusishe kwenye jambo lolote ambalo litaharibu sifa yako na jina lako. Usishiriki mpango wowote wa mkato wa kufikia mafanikio, mipango hii mingi siyo halali na itaishia kuharibu mafanikio yako.

Wapo ambao wanafanikiwa na kuwa matajiri kwa njia ambazo siyo halali, lakini hawawezi kujivunia utajiri huo mbele ya wengine. Kibaya zaidi utajiri wa aina hiyo umekuwa haudumu muda mrefu. Wewe huhitaji kupita njia hiyo, kwani unaweza kujijengea utajiri kwa njia za halali kabisa, ukianzia chini kabisa. Fanyia kazi mambo haya saba tuliyojifunza hapa na hakika maisha yako hayatabaki hapo yalipo sasa. Kama kuna ambavyo tayari unafanyia kazi, endelea kuboresha zaidi na vifanye kuwa misingi ya maisha yako.

Kama ungependa kujifunza zaidi sababu zinazokuzuia kufikia utajiri, soma kitabu KWA NINI MPAKA SASA WEWE SIYO TAJIRI. Kitabu ni softcopy na kinatumwa kwenye email, unasomea kwenye simu yako au kompyuta yako kama ulivyosoma makala hii. Gharama ya kitabu ni tsh elfu tano. Kukipata tuma tsh 5,000/= kwa simu namba 0755 953 887 au 0717 396 253 kisha tuma email yako na utatumiwa kitabu.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Makirita Amani,

Kupata blog yako ya kitaalamu, unayoweza kuitumia kutengeneza kipato, BONYEZA maandishi haya.

Kama umejifunza kupitia makala hii karibu tujifunze zaidi kupitia KISIMA CHA MAARIFA, ambapo utaingia kwenye kundi la wasap na kupata mafunzo kila siku. Bonyeza maandishi haya kujiunga na KISIMA CHA MAARIFA.
Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Pata kitabu BIASHARA NDANI YA AJIRA ujifunze jinsi unavyoweza kuanzisha na kukuza biashara yako, pia utajifunza mifereji nane(08) ya kipato unayopaswa kuwa nayo ili kufikia uhuru wa kifedha. Bonyeza maandishi haya kupata kitabu.

Viewing all articles
Browse latest Browse all 1010

Trending Articles



<script src="https://jsc.adskeeper.com/r/s/rssing.com.1596347.js" async> </script>