Katika maisha yako hakuna kitu ambacho unaweza ukakipata bure bila kulipia hiyo haiwezekani na haitakuja kuwezekana. Kil kitu unachokitaka ni lazima gharama ihusike ili ukipate, vinginevyo hutaweza kupata kile unachokihitaji katika maisha yako na utaishia kulalamika. Katika maisha yetu kumbuka tunalipia kodi, chakula, usafiri, pango na vingine chungu nzima, gharama hizi huhusika ili kuweza kupata kile tunachokihitaji.
Huu ni utaratibu ambao upo katika maisha ya binadamu ili aweze kupata kile anachokihitaji. Huwa kuna ulazima wa kulipia kitu husika, kinyume cha hapo huwa haiwezekani kupata kile unachokihitaji katika maisha yako. Ni gharama hizi ambazo huwashinda wengi na kusababisha kukosa kile wanachokihitaji na kuishi maisha magumu. Kama unataka kufanikiwa ni lazima ulipie gharama hizi. Gharama hizo ni zipi?
Hizi Ndizo Gharama Unazotakiwa Kuzilipia, Ili Uweze Kupata Kile Unachokihitaji Katika Maisha Yako.
1. Kukabiliana na vizuizi.
Kati ya gharama kubwa ambayo unatakiwa kuilipa na ambayo huwa inawashinda wengi na kujikuta wamefika mwisho wa safari yao ya mafanikio ni kukutana na vizuizi. Mara nyingi vizuizi hivi kwa wengi huwezi kufahamika kama matatizo au vikwazo. Hii ni gharama ambayo unatakiwa uitambue sasa kuwa unatakiwa kuilipia ili kufikia mafanikio makubwa unayoyataka. Wengi huwa wanakata tamaa sana wanapokutana na vizuizi katika safari yao ya mafanikio.
Kitu muhimu ambacho unatakiwa kujua hapa ni kuwa hakuna mafanikio ambayo unayeweza kuyapata burebure ama kiurahisi tu. Unapokutana na changamoto au tatizo, acha kulalamika wala kulaumu, hiyo kwako huwa ni ishara ya kukuonyesha kuwa unapaswa kulipia hiyo gharama, ambayo ndio tatizo lenyewe ili ufikie mafanikio yako. Na njia muhimu ya kulipia gharama hiyo ni kutatua tatizo hilo na kusonga mbele na sio kukimbia.
Kama unataka kufika juu kimafanikio jifunze kukabiliana na vizuizi vyovyote vile vinavyokukabili. Kwa jinsi utakavyokuwa unaweza kumudu kukabiliana na vizuizi hivyo, hivyo ndivyo utakavyokuwa unalipa gharama za kupata kile unachokihitaji. Na tunapozungumzia gharama hatumaanishi pesa tu ndio gharama peke yake, hapana. Huwa zipo gharama vnyingine ambazo unatakiwa uzilipie kama hizi ili kufika kwenye kilele cha mafanikio
2 . Kufanya kazi kwa bidii.
Hautaweza kupata kile unachokihitaji katika maisha kama utakuwa mtu wa kutokujituma na kutokufanya kazi kwa bidii kubwa. Maisha yako ili yaweze kuleta mafanikio kitu unachotakiwa kufanya sasa ni kujituma na kufanya kazi kwa bidii zote. Hii ni gharama ambayo huwezi kuikwepa hata ufanyaje, vinginevyo utabaki na utaendelea kuwa na maisha yaleyale magumu ambayo unayaishi.
Wengi huwa wanashindwa kulipia gharama hii ya kufanya kazi kwa bidii, nakujikuta tayari wameshajitoa nje ya mstari wa mafanikio. Inawezekana huna mtaji umekata tamaa hayo yote sawa, lakini kinachoweza kukutoa hapo ulipo na kukufikisha kwenye ngazi nyingine ya mafanikio ni kujituma bila kuchoka mpaka kuona matunda ya kile unachokitaka. Ukichukua uamuzi leo wa kulipia gharama hii uwe na uhakika utafanikiwa.
3 . Kukosolewa sana.
Kuna wakati katika maisha yako unaweza ukajikuta huna raha wala amani kutokana na kukosolewa sana na wengi kiasi cha kwamba na wewe kuanza kuhisi pengine hufai. Kama kitu hiki kimewahi kukutokea ama kinaendelea kutokea katika maisha yako, acha kujishitaki au kukata tamaa wala kugombana na mtu kwa lolote lile, hiyo ni gharama muhimu pia kwako ambayo unatakiwa kukabiliana nayo au kuilipa ili uweze kufanikiwa.
Utaweza tu kumudu ama kukabiliana na gharama hii endapo wewe mwenyewe utaweza kuwa chanya na kuweza kusimama imara na kutetea kile unachokifanya na unachokiamini kuwa ndicho kipo sahihi katika maisha yako bila kuyumbishwa na kitu chochote iwe kwa maneno au kitu kingine mpaka kufanikisha jambo lako. Lakini, kama utakuwa wa kukata tamaa sababu ya maneno, hutaweza kufika mbali, jiamini, kisha songa mbele.
4. Kuongeza maarifa.
Ili uweze kufikia maisha ya mafanikio unayoyataka ni muhimu sana kwako kujifunza kunoa na kuongeza maarifa yako kila siku kwa kadri unavyoweza. Hili ni jambo ambalo mara nyingi tumekuwa tukiliongelea mara kwa mara kupitia matandao huu wa AMKA MTANZANIA juu hasa ya umuhimu wa kujisomea kwa ujumla na faida zake katika maisha yako.
Kama zilivyo gharama nyingine ambazo zinaweza kukuwezesha kupata kile unachokihitaji, hata pia kuongeza maarifa ni moja ya gharama unazotakiwa kuzilipia ili kufika kule unakotaka kufika kimafanikio. Ni lazima kunoa ubongo ili kuweza kukabiliana na changamoto nyingi zinazokuzunguka. Unapokuwa unashindwa kujisomea maanake unakuwa unayaruhusu maisha yako kushindwa kiurahisi sana.
Kwa kifupi, katika maisha yako unaweza kukatishwa tamaa na mambo mengi yanayokuzuia wewe kufikia ndoto zako, lakini huo huwa sio mwisho wa mafanikio yako. Kwani huwa kuna njia muhimu ya kuyashinda yote hayo ambayo yanakuzuia kufikia mafanikio yako, njia hiyo ni kulipa gharama tu kama tulivyojadili. Kwa kulipa gharama utafika kule unakotaka katika maisha yako na hutakata tamaa tena ikisha tambua hilo kuwa kuna kulipa gharama. Lipia gharama kwa kile unachokihitaji ili utimize ndoto zako.
Kwa makala nyingine nzuri hakikisha unatembelea DIRA YA MAFANIKIO kwa elimu na maarifa bora yatakayoboresha maisha yako.
Nakutakia kila kheri endelea kutembelea AMKA MTANZANIA kwa kujifunza na kuhamasika kila siku.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
IMANI NGWANGWALU,
- 0713 048035,
- ingwangwalu@gmail.com